MTWARA MIKINDANI MANISPAA

Jumanne, 16 Januari 2018

 MTWARA-MIKINDANI YATUMIA SHILINGI MIL 834.1 KUTEKELEZA MIRADI YA MAENDELEO
Januari 16, 20180 Comments



Muonekano wa ndani wa jengo la machinjio ya Chuno baada ya kufanyiwa ukarabati kwa kutumia fedha za mapato ya ndani

Na Jamadi Omari


Katika kuhakikisha kuwa Manispaa Mtwara-Mikindani inaendelea kuboresha huduma za Jamii kwa Wananchi wake, imetoa na kutumia fedha kiasi cha shilingi milioni  834,074,361.79 kutoka katika mapato yake ya ndani Kutekeleza miradi mbalimbali ya Maendeleo, kuchangia mfuko wa Wanawake na Vijana pamoja na ulipaji fidia kwa wananchi.

Akizungumza Ofisini kwake mkurugenzi wa Manispaa Mtwara-Mikindani Bi Betarice Dominic amesema kuwa fedha ni mapato yatokanayo na kodi mbalimbali zinazolipwa na Wananchi na hivyo Manispaa imeona umuhimu wa kuzirudisha kwao ili kuimarisha miundombinu mbalimbali inayowagusa moja kwa moja.

Amesema kuwa Miradi iliyopelekewa fedha imegusa sekta mbalimbali zikiwemo sekta ya elimu, Utawala, Ufugaji na Uvuvi,Barabara,Afya pamoja na Kilimo. Aidha amewashukuru na kuwapongeza Wananchi  wa manispaa kwa kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi na kuwataka kuwa na utamaduni huo ili kuijenga Manispaa iliyo bora na yenye kuonekana.




 Jengo la mwalo wa Mikindani lililopo Kata ya jangwani likiwa kwenye hatua ya umaliziaji
 
Kwa upande wake Afisa Mipango wa Manispaa Ernest Mwongi amesema kuwa fedha zote zilizotolewa zimeshapelekwa kwenye Akaunti za miradi husika na kuna miradi mingine imeshatekelezwa na kukamilika, na miradi mingine  ipo kwenye hatua ya utekelezaji na kwamba  idara  ya mipango inahakikisha inaifuatilia kwa ukaribu miradi iliyobaki ili iweze kukamilika kwa wakati.

Ameitaja Miradi inayotekelezwa kulingana na fedha iliyotolewa ni pamoja na Mradi wa ujenzi  wa zahanati Mbawala chini, UKarabati wa Machinjio, Ujenzi wa matundu ya vyoo Shule ya Msingi Mbae na Mtawanya, Ujenzi wa Vyoo Shule za  Msingi Mjimwema, Shangani na Mlimani.

Miradi mingine ni Ujenzi wa Kalvati Miseti, Ununuzi wa pikipiki 5 kwa ajili ya watendaji wa Kata, Ununuzi wa gari la Mkurugenzi, Ujenzi wa Uzio  Ofisi kuu ya Manispaa, Ujenzi wa Shedi mwalo wa samaki Mirumba, Ununuzi wa gari la kufagia barabara pamoja na Ujenzi wa nyumba  za Wakuu wa Idara.

 Fedha hizo vilevile zimeelekezwa katika Ujenzi wa Ofisi ya Kata Mtawanya na Tandika, Umaliziaji wa ujenzi Ofisi ya Kata Jangwani, Ujenzi wa choo soko la kiyangu, Ujenzi wa nyumba za walimu Namayanga, Ujenzi wa soko la Mitengo, Uandaaji na ununuzi wa miche ya Korosho, Ununuzi wa mbegu za Mtama, uwekaji wa nguzo na minyororo barabara ya TANU, Ujenzi wa vyumba vya madarasa 3 Shule ya Sekondari Mitengo na Mangamba, Pia Utengenezaji wa madawati na uwekaji wa Taa Stendi kuu ya mabasi.



 Sehemu ya uzio wa jengo la ofisi kuu,ujenzi huo unaendelea

Asha Mapesa mkazi wa Chuno amepongeza Manispaa kwa kazi wanayoifanya ya kuleta maendeleo na kuahidi kutoa ushirikiano kwenye kulinda rasilimali hizo kwa manufaa yao na vizazi vijavyo.

Baada ya kufanya Mapitio ya bajeti 2017/2018 mwezi Desemba 2017, Manispaa Mtwara-Mikindani imepanga kukusanya bilioni 4,601,204,136 kutoka katika mapato yake ya ndani, Hadi Desemba 31,2017 Manispaa imekusanya bilioni 2,720,578,528 sawa na asilimia 59 ya bajeti iliyopangwa.

 Ujenzi wa matundu ya vyoo Shule ya Msingi Mtawanya ukiwa kwenye hatua za umaliziaji
Reading Time:

Jumatano, 3 Januari 2018

MANISPAA YAFIKIA ASILIMIA 93 UJENZI  WA KITUO CHA AFYA LIKOMBE
Januari 03, 20180 Comments






Jengo la nyumba ya mganga

Na Jamadi Omari

 Manispaa ya Mtwara-Mikindani Hadi kufikia Disemba 31,2017 imefikisha asilimia 93 ya ujenzi wa miundombinu ya afya katika kituo cha afya likombe  na kugharimu kiasi cha fedha shilingi milioni  326,457,759.18 kati ya milioni 500 zilizotolewa na Serikali kuu kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu hiyo.
Asilimia 7 iliyobaki inatarajia kukamilika baada ya wiki mbili kuanzia Januari 1,2018 na kwamba hadi kukamalika kwa mradi huo Manispaa imekadiria kutumia milioni 400 na kubakiwa na shlingi milioni 100 zitakazotumika  katika ujenzi  na ukamilishaji wa miundombinu mingine katika kituo hiko ikiwemo ukarabati wa jengo La OPD , Ujenzi wa choo cha wagonjwa wanaokuja kutibiwa kwenye kituo hicho ambacho kitagharimu Shilingi milioni 15.
Akizungumza kwenye ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa mradi huo iliyofanyika Januari 1,2018 kati ya Timu ya ukaguzi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara na Timu ya Menejiment ya halmashauri Mkurugenzi wa Manispaa Bi Beatrice R. Dominic amesema kuwa Ujenzi wa mradi wa miundombinu ya afya  unaendelea vizuri na kwa gharama inayoridisha.
Akielezea kuhusu mikakati iliyotumika katika ujenzi huo hadi kupelekea kukisia kubakiwa na fedha zilizotajwa Beatrice amesema kuwa Ofisi yake imetii  agizo la Serikali lililotaka mradi huo kujengwa kwa kutumia mafundi wenyeji  ambao wametoa gharama za ujenzi zilizo halisi na kazi imekuwa nzuri,na kwamba kila jengo amepewa fundi mmoja  na vibarua wake.
Ameongeza kuwa Menejimenti ya halmashauri ilikubaliana vifaa vyote vya ujenzi vinunuliwe viwandani ikiwemo mabati,Gypsum,Tiles,rangi,cable za umeme na vifaa vingine  ili kuweza kupunguza gharama na vifaa vichache vilinunuliwa kwenye eneo la Manispaa pamoja na mafundi waliojenga majengo hayo.

Aidha amesema kuwa mradi umefikia hapo kwa kuwa kulikuwa na umakini mkubwa kwenye usimamizi na kwenye kufanya makadirio  Lakini pia ushirikiano ulikuwa mkubwa kati ya timu ya halmashauri na Timu ya uendeshaji wa kituo.

Nae Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara Duncan Thebas amepongeza Manispaa kwa kazi nzuri iliyofanyika na kwamba inadhihirisha maamuzi sahihi ya Serikali ya kuikomboa Tanzania kwa kutumia mafundi wenyeji kwenye ujenzi wa miundombinu hiyo. Aidha amepongeza ujenzi wa njia za kupita(walk way) ambayo kwenye maelekezo ya mradi haikuwepo lakini Manispaa imeona umuhimu wa kujenga .


 

 Jengo la wodi ya Mama na Mtoto


Kaimu Mganga Mkuu wa Manispaa DR.Christa Nzali ameishukuru Serikali kwa kuleta fedha hizo kwani kukamilika kwa majengo hayo kutasaidia kutatua changamoto zinazowakabili ikiwemo kupunguza vifo vya akina mama na watoto, kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali ya Mkoa.

Wakati huo huo Fundi aliyepewa kazi ya ujenzi wa Wodi ya  Mama na Mtoto Athumani Bandiko ameishukuru Serikali kwa kuwapatia kazi ya ujenzi kwani imewapa nafasi ya wao kuonesha uwezo wao kama mafundi wadogo lakini pia imesaidia kutengeneza ajira kwa vijana. AIdha ameiomba Serikali iwaamini na iendelee kuwapa kazi katika majengo mengine.

 Manispaa Mtwara-Mikindani Oktoba 13,2017 ilipokea fedha kiasi cha shilingi 500 kutoka Serikali kuu kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya afya katika Kituo cha afya Likombe, Miundombinu iliyojengwa ni pamoja na Wodi ya Mama na Mtoto, Maabara, Chumba cha kulaza Maiti, Chumba cha Kufulia nguo, Kichomea taka pamoja na ujenzi wa Nyumba ya Mganga.

 

 Timu ya Ukaguzi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Timu ya Menejiment wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kumaliza ukaguzi





Reading Time:
Copyright: mtwaramikindanimc©2018